Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa maagizo kwa viongozi na watendaji wa halmashauri za Wilaya ya Itigi na Manyoni kuhakikisha kuwa hoja zote za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinazotokana na mapungufu ya ndani zinatekelezwa kwa weledi na kufutwa kabisa.
Akizungumza katika vikao maalum vya mabaraza ya madiwani vya kupitia taarifa ya utekelezaji wa hoja za ukaguzi kwa mwaka wa fedha, Mhe. Dendego alisema kuwa ni aibu kwa halmashauri kuendelea kuwa na hoja zinazoweza kuzuilika kwa nidhamu na uwajibikaji wa ndani. Alieleza kuwa hatua kubwa ya mabadiliko inaonekana, hasa kwa Halmashauri ya Itigi iliyopunguza hoja kutoka 40 hadi 11, akisisitiza kuwa juhudi hizo ziimarishwe zaidi hadi kufikia hoja sifuri.
Kadhalika ameipongeza Itigi kwa kiwango kizuri cha ukusanyaji mapato ya asilimia 98.7 na kuelekeza kifikie asilimia 100, sambamba na kuhakikisha fedha za lishe na asilimia 10 kwa wanawake zinatumika kwa wakati na ufanisi. Aidha, alitoa maagizo kwa halmashauri zote kukata mishahara ya watumishi waliokopeshwa na hawajarejesha, huku akielekeza kuwa fedha zote za miradi ya maendeleo ziheshimiwe na kutumika kikamilifu ndani ya mwaka wa fedha.
Mhe. Dendego pia amewataka madiwani kuhakikisha wanasimamia kikamilifu matumizi ya rasilimali na miradi ya wananchi, huku akiwataka watendaji kuhakikisha mifumo ya ndani ya usimamizi wa fedha inaimarika na kuwa endelevu akisisitiza kuwa lengo la Mkoa wa Singida ni kuwa na halmashauri zenye hoja chache au sifuri, jambo linalowezekana kwa mshikamano kati ya watendaji na viongozi wa kisiasa.
Akizungumza katika kikao hicho,Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema kuwa Itigi imefanya vizuri katika kushughulikia hoja na kwamba hatua hiyo ni mfano kwa halmashauri nyingine huku akisisitiza umuhimu wa kujaza mfumo wa PEPMIS kwa wakati ili watumishi stahiki wapate fursa za kupandishwa vyeo kwa haki.
Kadhalika amehimiza Halmashauri kuangalia fursa mpya za kiuchumi kwa kuanzisha kampuni maalum (SPV) itakayowezesha halmashauri kunufaika na mapato mapya kupitia miradi rafiki kwa mazingira kama vile biashara ya hewa ya ukaa. Dkt. Mganga alisema kuwa mabadiliko ya kimfumo ni lazima yasimamiwe kisera lakini pia kwa ubunifu wa ndani katika vyanzo vya mapato visivyo tegemezi.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Mhe. Hussein I. Simba, amesema kuwa mwelekeo ulioasisiwa na Mkuu wa Mkoa umeifanya halmashauri kuwa makini katika usimamizi wa hoja na kutumia vikao vya kisekta na kamati za ndani kufuatilia kila hoja hadi kufikia utekelezaji wake.
Amesema kuwa dhamira ya halmashauri ni kufuta kabisa hoja zote kabla ya ukaguzi unaofuata.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Ayoub Juma Kambi, alisema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya ofisi yake na madiwani umechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza hoja na kutekeleza maagizo yote ya ukaguzi. Alibainisha kuwa fedha za lishe zilitumika kikamilifu na kuwa asilimia 10 kwa wanawake zimeshapokelewa na vikundi husika kwa matumizi ya maendeleo.
Katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Mkuu wa Mkoa aliwataka madiwani na watendaji kuendeleza nidhamu ya ufuatiliaji wa hoja, huku akipongeza hatua ya halmashauri hiyo kupata hati safi. Alielekeza kuwa ni wakati sasa wa Manyoni kuongoza kwa kuzuia kabisa hoja mpya kupitia mifumo thabiti ya usimamizi.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Mhe. Jumanne Shabani Mlagaza, alisema kuwa halmashauri yake imejipanga kuhakikisha hoja zote zilizobaki zinapewa kipaumbele na kutatuliwa kwa wakati akisema kuwa ni wakati wa kuacha kuwa wabobezi wa kujibu hoja na badala yake kuwa viongozi wa kuzuia hoja mapema.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, alisema kuwa lengo la mkaguzi si kuadhibu bali kuimarisha mifumo ya usimamizi wa fedha na utawala bora huku akisitiza kuwa Halmashauri zinapaswa kutumia taarifa ya ukaguzi kama kioo cha kuonyesha maeneo ya kuboresha na kuhakikisha mikopo inayotolewa inarejeshwa ipasavyo kwa ajili ya ustawi wa wananchi wote.
Vikao hivyo vya Itigi na Manyoni vimeweka msingi wa mwelekeo mpya wa uwajibikaji, nidhamu, na mabadiliko ya kiutendaji katika usimamizi wa fedha za umma, vikiwa ni kielelezo cha dhamira ya Mkoa wa Singida kuhakikisha maendeleo yanatokana na uwazi, weledi, na usimamizi makini wa rasilimali za wananchi.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.