Maafisa ugani wa mkoa wa Singida wametakiwa kuandaa na kutekeleza mpango mkakati unaosomana na unaotekelezeka kwa lengo la kuwafikia wakulima kwa ufanisi, hususan katika utoaji wa elimu sahihi na yenye usawa kuhusu mfumo wa stakabadhi za ghala.

Hayo yamesemwa leo katika ukumbi wa mkuu wa mkoa wa Singida na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa, Bw.Pancras Stephen wakati wa kikao kazi kilichowakutanisha Maafisa Ugani, COPRA na wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, kikao kilicholenga kuwajengea uwezo washiriki kuhusu majukumu ya COPRA na kuwawezesha Maafisa Ugani kutoa elimu kwa wakulima ili kuboresha uzalishaji na upatikanaji wa mazao ya kutosha shambani.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Pancras amesisitiza kuwa mpango kazi unaotarajiwa kutumika unapaswa kuwa wa pamoja na unaoendana katika maeneo yote ya utekelezaji, ili kuhakikisha elimu inayotolewa kwa wakulima inakuwa na mwelekeo mmoja, hasa katika matumizi ya mifumo inayohusiana na stakabadhi ghalani.
Ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mkulima hapunjwi, mapato hayapotei na mauzo ya mazao yanafanyika kwa uwazi na ufanisi, akiongeza kuwa sekta ya kilimo ina mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kwa kuiwezesha Serikali kupata mapato ya kugharamia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa dawa za hospitali, ulipaji wa mishahara na utekelezaji wa huduma nyingine za kijamii.

Aidha, amewataka Maafisa Ugani kuzingatia misingi ya maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kujiepusha na vitendo vyovyote visivyoendana na maadili ya Utumishi wa Umma, huku akiwahimiza kuyazingatia kikamilifu mafunzo na miongozo inayotolewa na COPRA.
"Mzingatie maadili ya kazi, hakikisheni mnajiepusha na vitendo vyovyote vile ambavyo mnaona kwamba haviendani na utumishi wa umma, kugombana na wananchi, ukiwaheshimu kulingana na siasa zao ukiwaheshimu kulingana na shughuli zao za kila siku huo mradi utabakia kwenye utaalamu." Alisema

Na kwa upande wake Meneja wa COPRA kanda ya kati,Bw.Andrew Mgaya amefafanua kuwa kabla ya kuanzishwa kwa mfumo wa stakabadhi za ghala, gharama za ukusanyaji wa tozo mbalimbali zilikuwa kubwa, hata hivyo kuanzishwa kwa mfumo huo kumechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza gharama hizo kutokana na matumizi ya mifumo ya kidijitali inayorahisisha ukusanyaji wa mapato.

"Ninyi nyote mnafahamu Mazao yake yaliyopo kwenye stakabadhi za ghala mnafahamu hali iliyokuwepo awali na hali iliyokuwepo kwa sasa, ninyi kama Halmashauri kule uwezo wa kukusanya zile sese zimepungua kidogo kwa sasa inapatikana kwenye mfumo."
Ameongeza kuwa lengo la kikao hicho pia ni kuwasilisha na kueleza miongozo mbalimbali iliyoandaliwa na COPRA kuhusu usimamizi wa mazao tofauti, kwa nia ya kuhakikisha mazao mengi zaidi yanaingizwa katika mfumo wa stakabadhi za ghala ili kuongeza thamani, uwazi na ushindani wa mazao ya wakulima sokoni.

Kwa upande wake, Afisa Ugani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, Bw. Samweli Vedasto, amesema kuwa baada ya mafunzo hayo, Maafisa Ugani wako tayari kwenda kuwafikia wakulima kwa kutoa elimu ya kina kuhusu mfumo wa stakabadhi za ghala kupitia mikutano mbalimbali itakayofanyika katika ngazi ya vijiji na kata, ili kuhakikisha wakulima wengi zaidi wanaufahamu na kuutumia mfumo huo kwa tija.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.