Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego ametoa wito kwa Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na wadau wa maendeleo kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya kilimo ili kuhakikisha matokeo chanya na endelevu kwa wananchi.

Ameyasema hayo Februari 6, 2026 wakati wa kikao kazi cha tathmini ya utendaji wa wadau wa mradi unaotekelezwa na Shirika la HELVETAS, kilichofanyika katika Ukumbi wa Amenity Hotel, Manispaa ya Singida.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Dendego ameeleza kuwa taarifa na takwimu zinazowasilishwa na wadau wa maendeleo ni nyenzo muhimu katika kupanga na kutekeleza mipango ya Serikali, hivyo zinapaswa kuchambuliwa na kuingizwa kikamilifu katika mipango ya Halmashauri na Mkoa. Amesema hatua hiyo itawezesha kufanya tathmini ya kina ya mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizopo na mwelekeo wa maendeleo, sambamba na kuboresha utoaji wa huduma kwa wakulima na wadau wa sekta ya kilimo.

Aidha, amesisitiza kuwa Serikali ina wajibu wa kuhakikisha miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau kama HELVETAS inasimamiwa ipasavyo na kurasimishwa katika mifumo ya Serikali ili matokeo yake yaendelee kuwafaidisha wananchi hata baada ya kukamilika kwa miradi husika. Ameeleza kuwa jitihada hizo zina mchango mkubwa katika kuimarisha kilimo endelevu, kuongeza uzalishaji, kulinda mazingira na kuchochea maendeleo ya kiuchumi mkoani Singida.

Vilevile, amewahimiza wakulima, wajasiriamali na wananchi kwa ujumla kutumia ipasavyo elimu na teknolojia wanazopewa kupitia miradi ya maendeleo, akisisitiza umuhimu wa ubunifu, uchapakazi na uwajibikaji akisema kwa kufanya hivyo, Mkoa wa Singida utaendelea kupiga hatua katika uzalishaji wa kilimo, uanzishaji wa viwanda vidogo na kuongeza fursa za ajira kwa wanawake, vijana na makundi yenye mahitaji maalum, hatua itakayochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya Mkoa.

Kwa upande wake, Afisa kutoka Shirika la HELVETAS mkoani Singida amesema shirika hilo linaendelea kutekeleza miradi inayolingana moja kwa moja na vipaumbele vya Mkoa wa Singida, hususan katika maeneo ya kilimo endelevu na uchumi wa kijani, uwezeshaji na uhifadhi wa rasilimali za asili pamoja na uwezeshaji wa wanawake na vijana kiuchumi.

“HELVETAS inalenga pia kuimarisha ushiriki wa wananchi katika mipango na maamuzi ya maendeleo ili kujenga jamii zinazojitegemea, zenye ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na zinazoshiriki kikamilifu katika maendeleo endelevu ya Mkoa wa Singida.” Amefafanua.
Na kwa upande wa wadau waliohudhuria kikao hicho, wamesema mradi wa HELVETAS umewajengea uwezo mkubwa katika uzalishaji na uongezaji thamani wa mazao. Wameeleza kuwa kupitia mafunzo waliyopata wamejifunza mbinu bora za kilimo, utengenezaji wa mbolea na usindikaji wa mazao, hali iliyowawezesha kuongeza tija shambani na kuboresha ubora wa bidhaa zao.

“Kupitia mradi wa HELVETAS tumepata elimu nyingi ikiwemo mbinu bora za kilimo na usindikaji. Kwa sasa tuna kiwanda kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kinachotusaidia kusindika bidhaa zetu, na tukipata ithibati ya TBS tutaweza kupanua masoko yetu ndani na nje ya Mkoa.” wamesema.

Kikao hicho ni jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, likiwa na lengo la kuharakisha maendeleo ya sekta ya kilimo, kuongeza kipato cha wananchi na kuifanya Singida kuwa mkoa wa mfano katika utekelezaji wa kilimo endelevu na uchumi wa kijani.



SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.