Mkoa wa Singida unakwenda kunufaika na umeme katika vitongoji vyake vyote ,ikiwa ni mpango wa Serikali kupitia Wakala wa Nishati vijijini(REA) katika mradi wa ujazilizi fungu la 2(a) ambapo mpaka kukamilika kwake utafikia kaya 13,259.

Hayo yamezungumzwa wakati Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego alipowapokea wakandarasi waliofika kwa ajili kuanza mradi huo ambao ni China Railway No.4 Engineering Group Ltd unaogharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 45.7 kutoka Serikali kuu.
Akizungumza,Mhandisi Thomas Mbaga ambae Kaimu Mkurugenzi Umeme Vijijini kutoka REA, amesema kuwa mkoa wa Singida unakwenda kuwa mnufaika wa mradi huo wa umeme ambapo vitongoji 376 vitakwenda kufikiwa na huduma hiyo.

Sambamba na hilo,amesema kuwa kupitia mradi huo wananchi ambao watakua bado kupata huduma ya 'wiring' watapata huduma hiyo kupitia program ya 'umeme tayari' ambayo mwananchi atapatiwa umeme kwa gharama ya Shilingi 27,000 pekee.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Dendego ameahidi ushirikiano wa kutosha kwa wakandarasi hao muda wote watakapokua wakitekeleza mradi huo Mkoani hapa akilenga kuhakikisha wananchi katika vitongoji vyote wanafikiwa na umeme kwa asilimia mia moja.
Kadhalika amewataka wananchi kutumia fursa hiyo vizuri bila kubaki nyuma akisisitiza kuwa hiyo itakuwa mojawapo ya fursa ya kuwainua kiuchumi kutokana na fursa nyingi zitakazojitokeza baada ya kupata umeme ikiwemo maendeleo ya viwanda vidogo na vikubwa

Mpaka sasa,jumla ya vitongoji 1,052 kati ya 2,289 Mkoani Singida vimekwisha kupata umeme.

SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.