Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene, amewataka wahitimu katika vyuo mbalimbali nchini kuepuka na vitendo vya rushwa na ufisadi wanapoajiriwa kwenda kufanya kazi kwakuwa mambo hayo yanaleta madhara katika ufanisi wa utendaji kazi wa Serikali.
Alisema hayo leo wakati akizungumza na wanafunzi, watumishi na wananchi katika sherehe za mahafali ya 41 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Singida ambapo jumla ya wanafunzi 1330 walihitimu na kutunukiwa vyeti katika ngazi mbalimbali.
“Sote tunaohitimu katika vyuo vyote nchini mnapofikilia kwenda kufanya kazi serikalini mhakikishe mnakuwa wasimamizi na watunzaji wa maadili lakini pia mhakikisha mnatunza siri za serikali na mtaepuka rushwa na ufisadi na mambo mengine ambayo yanaleta madhala katika ufanisi wa utendaji kazi wa serikali,” alisema.
Simbachawene amesema duniani kote pamoja na kuwepo kwa rasilimali nyingine lakini raslimali muhimu ni watumishi wa umma ambao wanapaswa kupata mafunzo kabla na baada ya kuanza kazi ili kuwajengea uwezo wa utendaji mzuri wa kazi.
“Wakati mwingine tunalaumiana juu ya uwezo mdogo wa kiongozi wa chini lakini kumbe hawajapata mafunzo jinsi ya kuwahudumia wananchi, niwakumbushe na niwasisitize kwamba watumishi wa umma mnalo jukumu kubwa katika mchango wa maendeleo ya nchi, muhimu hapa ni kuhakikisha mnatunza maadili ya kazi,” amesema.
Simbachawene amesema nchi yetu ni kubwa ina wananchi wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali lakini ipo migogoro mingi hasa ya ardhi, hivyo watumishi wa umma hususani maafisa watendaji wa vijiji, kata na tarafa wakijengewa uwezo jinsi ya kutatua migogoro itapungua na wananchi wataendelea na shughuli nyingine za uzalishaji badala ya kupoteza muda mwingi kwenye migogoro.
Aliongeza kuwa Serikali inayo matarajio makubwa na Chuo cha Utumishi wa umma na wahitimu wake katika kuhakikisha wanajenga uwezo na umahiri katika katika kutekeleza majukumu yao wanapokuwa kazini.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt.Fatuma Mganga akizungumza katika mahafali hayo,Amewahimiza Wahitimu kutobweteka badala yake wajiendeleze katika fani zingine zinatolewa VETA ili waweze Kujiajiri.
"Sio dhambi kwa mtu aliemaliza Chuo cha utumish kujifunza fani mbali mbali,VETA kuna juzi nyingi,tusiende kukunja mikono na kuilaumu Serikali,kila mmoja ajishughulishe.Anaetaka ujuzi wa ufundi nenda kajiunge na VETA upate ujuzi wako wakati unasubiri ajira"amesema Daktari Mganga.
Naye Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dk. Ernest Mabonesho, amesema katika mafunzo ya muda mrefu chuo kimedahili wanafunzi 10, 507 katika ngazi mbalimbali na katika mafunz ya muda mfupi kimeweza kuwajengea uwezo watumishi 11,122 mpaka sasa na wale waliopewa mafunzo ya awali.
Amesema katika mwaka huu wa fedha unaoisha chuo kimefanya tafiti sita ambazo zipo hatua ya mwisho kukamilisha ambazo zinaangalia changamoto za uongozi katika usimamizi na ufanisi wa taasisi za umma na ufanisi wa mafunzo kwa watumishi wa umma katika kuwezesha kutoa huduma.
Dk.Mabonesho amesema tafiti nyingine zinazofanyika ni kuangalia maeneo ya Teknolojia na mabadiliko ya stadi katika kada ya uhazini, matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa shughuli za kiofisi,matumizi ya mfumo wa manunuzi wa kielektroniki katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi na ufanisi wa utoaji wa huduma kwa upande wa Serikali za mitaa.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.