Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amesema Mkoa wa Singida umejipanga kikamilifu kuhakikisha unaongoza kitaifa katika viwango vya ufaulu kwa shule za msingi, sekondari na vyuo, kupitia ushirikiano wa pamoja kati ya serikali, walimu, wazazi na wadau wote wa elimu.
Mhe. Dendego ameeleza kuwa Mkoa wa Singida umeendelea kupokea uwekezaji mkubwa kutoka Serikali Kuu, ikiwa ni pamoja na zaidi ya Shilingi bilioni 40 kwa ajili ya elimu bila malipo na zaidi ya bilioni 70 kwa ujenzi wa miundombinu.
"Singida imepokea zaidi ya Shilingi bilioni 40 kwa ajili ya elimu bila malipo na zaidi ya Shilingi bilioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya elimu, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa shule mpya 12 za msingi, shule 34 za sekondari, shule za amali katika kila halmashauri, pamoja na miundombinu ya Chuo cha Utumishi wa Umma"amesema Mhe.Dendego
Dendego amesema mazingira ya kufundishia na kujifunzia yameendelea kuboreshwa kwa kasi kubwa, walimu wanafanya kazi kwa weledi na wanafunzi wanaendelea kufanya vizuri. Ametoa wito kwa jamii kushirikiana na serikali katika kutatua changamoto zinazoikumba sekta hiyo, ikiwemo utoro wa wanafunzi na mimba za utotoni.
Aidha, amepongeza walimu kwa kazi kubwa wanayoifanya, akibainisha kuwa mafanikio ya ufaulu katika mitihani ya darasa la 4, 7, kidato cha 2, 4 na 6 yameendelea kuongezeka, kutokana na juhudi za walimu na mazingira bora ya kujifunzia yaliyoboreshwa.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema kikao cha wadau wa elimu kimeitishwa kwa lengo la kutathmini mafanikio na changamoto zilizopo, na kuweka mikakati thabiti ya kuinua kiwango cha elimu mkoani humo. Amesisitiza kuwa mkoa unahitaji kujua ni kiasi gani umefanikiwa kutumia rasilimali ilizopatiwa na serikali, pamoja na mchango wa wadau mbalimbali kwa kuwa mnufaika mkubwa wa fedha za serikali na wadau wa maendeleo katika sekta ya elimu.
"Tunaendelea kushuhudia maboresho makubwa katika miundombinu, ajira za walimu na ongezeko la wanafunzi. Hiki kikao ni jukwaa la kupashana habari kuhusu mafanikio yaliyopatikana na hatua zinazofuata," amesema.
Naye Afisa Elimu wa Mkoa, Dkt. Elipidius Baganda akisoma taarifa, amesema Mkoa wa Singida una Shule za Msingi 709 na Sekondari 204, Vyuo vya ualimu viwili, Vyuo vya afya saba, vyuo vya maendeleo ya jamii viwili, Vyuo vya VETA viwili, Chuo cha Utumishi wa Umma, Chuo cha Uhasibu, na Chuo Kikuu kimoja.
Amesema licha ya mafanikio makubwa katika elimu ya sekondari, mkoa bado unakabiliwa na changamoto ya upungufu wa walimu, ambapo mahitaji ni zaidi ya walimu 9,000 huku waliopo wakiwa ni 5,000. Vilevile, amebainisha kuwa hali ya ufaulu katika elimu ya msingi haiko kwenye kiwango kinachoridhisha, na hivyo kuna haja ya kuongeza juhudi zaidi.
Wadau mbalimbali wa elimu kutoka halmashauri zote, waratibu wa elimu, walimu wakuu, wakuu wa shule na viongozi wa serikali wamehudhuria kikao hicho na kujadili kwa pamoja namna bora ya kuboresha elimu katika Mkoa wa Singida.
Mkutano huo umehitimishwa kwa wito kwa wadau wote kushirikiana kuboresha sekta ya elimu, ili Singida iweze kufikia nafasi ya juu kitaifa.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.