Mkuu wa Mkoa Mhe. Halima Dendego amehitimisha rasmi mfululizo wa mikutano ya Mabaraza ya Madiwani katika halmashauri zote saba za Singida kwa kusisitiza kuwa hakuna hoja itakayoachwa bila kushughulikiwa na hakuna hoja mpya itakayozalishwa.
Mhe. Dendego amesema kuwa hakuna hoja yoyote inayopaswa kuachwa ikiwa haijashughulikiwa ndani ya muda uliopangwa, huku akisisitiza kuwa halmashauri zote zinapaswa kuhakikisha zinafunga hoja zilizopo na kuzuia kuzalisha hoja mpya kwa kuboresha mifumo ya udhibiti wa ndani.
Akihitimisha mfululizo wa vikao vya Mabaraza ya Madiwani katika halmashauri saba za mkoa huo kwa kushiriki Baraza la Iramba, amesisitiza kuwa kila kiongozi na mtendaji lazima abebe jukumu lake kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa tija.
Kadhalika,amesema kuwa ni wajibu wa kila mtendaji kuhakikisha anatekeleza majukumu kwa ukamilifu, hususan katika kipindi hiki ambapo madiwani wanakwenda kwenye likizo fupi kuelekea uchaguzi. Amesema kuwa mafanikio ya kufikia “single digit” kutoka zaidi ya hoja 300 ni hatua kubwa na ya kujivunia, na sasa ni wakati wa kuhakikisha kile kilichobaki kinashughulikiwa kikamilifu.
“"Hakuna kuacha Kiporo katika kipindi hiki ambacho Wenzetu madiwani wanaenda likizo fupi kuelekea katika kipindi cha Uchaguzi mkuu 2025, basi Mkurugenzi na Wakuu wa Idara tuhakikishe yale yote waliyotuagiza wale waiyotuachia tunayatekeleza ili wananaporudi wakute tumeyatekeleza yote na tumevuka hatua kubwa." amesisitiza huku akiwatakia kila la heri madiwani wote katika kipindi cha uchaguzi huku akipongeza kazi iliyofanyika katika kata zote, akisema, “Yale mliyoyafanya yanaonekana, wala hayahitaji miwani kuyaona.”
Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi wa Mkoa Bw. Shaban Mongo Mongo amesema kuwa hoja zilizobaki katika Halmashauri ya Iramba ni mapinduzi makubwa ambayo yamepatikana kwa jitihada za pamoja za watendaji, viongozi na usimamizi wa karibu wa viongozi wa kitaifa akisesema kuwa hatua inayofuata ni kuhakikisha vielelezo vyote vinavyohitajika vinawasilishwa kabla ya tarehe 15 Julai 2025 ili ziweze kufungwa rasmi.
Amehimiza kuwa ili kuepuka kuzalisha hoja mpya, mifumo ya ndani ya udhibiti lazima iimarishe kwa kuanzia na maadili ya viongozi, ukaguzi wa ndani na uadilifu wa kila idara.
Katika suala la mapato, amesisitiza kuwa halmashauri inapaswa kufikia asilimia 100 ya makusanyo na kuhakikisha kuwa wadaiwa wa mikopo ya vikundi wanarudisha fedha hizo kwa wakati ili ziweze kutumika tena kwenye miradi mingine ya maendeleo.
Kwa upande mwingine Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa Bw. Othman Mwinjuma Jumbe amesema kuwa mapendekezo ya ukaguzi yamezingatiwa, na utekelezaji wake umeleta mabadiliko yanayoonekana. “
Amewaasa viongozi watumie mafanikio ya sasa kama msingi wa maendeleo endelevu kwa wananchi wake akiwataka watendaji kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uaminifu na kuimarisha utawala bora.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Iramba Bwa. Michael Matomora amesema kuwa maelekezo yote yaliyotolewa na Mhe. Halima Dendego yamepokelewa na watatekelezwa kwa ukamilifu kwa kushirikiana na timu nzima ya menejimenti.
Amesema kuwa hoja zilizobaki zitafanyiwa kazi kwa kina ili kuhakikisha zinafungwa ndani ya muda uliopangwa.
"Watumishi wa umma wanatekeleza ilani ya serikali iliyopo madarakani, na hivyo ni wajibu wao kuwasilisha matokeo yanayoonekana kupitia miradi ya maendeleo"amesema
Ameongeza kuwa wakati madiwani wakiwa kwenye likizo ya uchaguzi, menejimenti itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi kwa kufuata taratibu, sheria na miongozo yote ya serikali kwa heshima na uwadilifu mkubwa.
Kwa mujibu wa maelekezo ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI, mabaraza yote ya madiwani nchini yanavunjwa rasmi tarehe 20 Juni 2025. Baraza la Halmashauri ya Iramba limehitimisha mfululizo wa vikao vya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali katika halmashauri zote saba za Singida. huku Mhe. Dendego akihudhuria mabaraza yote hayo kama mgeni rasmi, na kuhakikisha kuwa kila Halmashauri inachukua hatua za dhati kuhakikisha hoja zote zilizopo zinafungwa, na hakuna hoja mpya inazalishwa, ili kulinda fedha za umma na kuongeza kasi ya maendeleo.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.