Spika wa Bunge Mstaafu Mhe. Anne Semamba Makinda amesema wanawake hawapaswi kuwa watu wa kusubiri kuletewa fursa, bali wanapaswa kujitokeza kuzitafuta kwa bidii, ujasiri na malengo ya kweli ya maendeleo.
Akizungumza kama mgeni rasmi katika kongamano la wanawake wa Mkoa wa Singida lililofanyika katika Kanisa la Unyankindi SDA, leo Juni 20,2025 Mhe. Makinda amewasihi wanawake wa Singida kuwa na moyo wa uthubutu na kuachana na kasumba ya kungoja kusaidiwa kila hatua.
Amesema kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameonesha njia na kuweka mazingira mazuri ya maendeleo, hivyo wanawake sasa hawana sababu ya kukaa pembeni.
“Wanawake jasiri hawangoji kuletewa, wanatafuta. Tusiwe watu wa kulalamika, bali tuwe watu wa kuchukua hatua,” amesema Makinda huku akisisitiza kuwa mitaji na nafasi za uongozi zipo, kinachohitajika ni ujasiri wa kuzifuata.
Amesema kuwa wanawake wa Singida wamekuwa mfano bora kwa Tanzania kwa kuwa mstari wa mbele katika uongozi na kushiriki kwenye maendeleo na kuwasihi kuchukua fomu kugombea nafasi mbalimbali na kuacha hofu ya kushindwa. Kadhalika Amewakumbusha pia wanawake kulinda kadi zao za kupigia kura kwa sababu hiyo ndiyo silaha ya ushindi wa viongozi wanaowataka.
Mhe. Makinda amesema mafanikio ya Rais Samia katika maeneo ya afya, nishati safi, elimu na miundombinu ni ushahidi kuwa mwanamke anaweza. Amesema uwekezaji mkubwa katika nishati safi umeokoa maisha ya wanawake waliokuwa wakiteseka na madhara ya kuni na mkaa.
“Leo, kwa sababu ya gesi, wanawake wanapika salama na wana muda wa kufanya kazi nyingine, hii ni hatua kubwa sana katika kuwawezesha wanawake,” amesema huku akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila mwanamke kusimama na kuunga mkono jitihada hizo kwa vitendo.
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amesema kongamano hilo ni ishara ya mshikamano, mshindo na mwamko wa wanawake wa Singida akisema kuwa maneno ya Mhe. Makinda katika kongamano la uchaguzi yaliyopita yamezaa matunda kwani wanawake zaidi ya 900 walijitokeza kugombea uongozi katika uchaguzi wa serikali za mitaa, na 109 kati yao walichaguliwa. “Hili ni onyesho kuwa wanawake wa Singida hawangoji kuletewa, wanajitokeza kuchukua nafasi zao kwa ujasiri,” amesema.
Amesema Mkoa wa Singida umefaidika sana katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita kupitia sekta za afya, elimu, miundombinu na huduma za jamii. Ameeleza kuwa zaidi ya vituo vya afya 80 vimejengwa, hospitali mpya nne zimeanzishwa, dawa na vifaa tiba vinapatikana kwa 95% na madaktari bingwa wametumwa kwa awamu tatu kutoa huduma kwa wananchi. Katika sekta ya maji, miradi 39 inatekelezwa na miundombinu imeimarishwa kwa kiwango cha lami, huku vijiji 100% vikiwa vimefikiwa na huduma hiyo muhimu.
Kadhalika Mhe. Dendego amesema Mkoa wa Singida umejipanga kutekeleza kikamilifu mpango wa matumizi ya nishati safi ambapo kila mwanamke atafikiwa akieleza kuwa kwa sasa majiko ya gesi yanapatikana kwa bei ya ruzuku ya shilingi 20,800 badala ya shilingi 48,000 huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kubeba maoni na changamoto zilizotolewa na wanawake hao kwenye kongamano hilo, hasa kuhusu upatikanaji wa mikopo, majiko ya gesi, na elimu ya ujasiriamali.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa kongamano hilo, akiwemo Mama Halima Hassan, ameshauri Serikali kurahisisha masharti ya mikopo kwa wanawake na kupeleka majiko ya gesi hadi vijijini ili kuwanufaisha wanawake walio wengi akisema kuwa wanawake wengi wana uwezo wa kufanya maendeleo endapo mifumo ya mikopo itaboreshwa na majiko ya ruzuku kufikishwa kirahisi.
Sofia Kabarata na Farida Budo wameongeza kuwa wanawake wanapaswa kushikamana, kuungana na kuungana kisera pale mwanamke anapojitokeza kugombea nafasi yoyote ya uongozi. Wametoa wito kwa wanawake wote kutimiza wajibu wao wa kikatiba kwa kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi ujao kwa kupiga kura na kuchagua viongozi wanaowaamini.
Wanawake wa Mkoa wa Singida wametumia kongamano hilo pia kumpatia Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan zawadi ya tuzo maalumu kama ishara ya kumpongeza na kumtambua rasmi kuwa kinara wa matumizi ya nishati safi nchini Tanzania, hatua inayowawezesha wanawake kuishi kwa usalama, afya bora na kuokoa muda katika shughuli za kila siku.
Kongamano hilo limefanyika kwa hamasa kubwa likiwa ni sehemu ya kusherehekea mafanikio ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuongoza taifa kwa ujasiri, maono na mshikamano, huku wanawake wa Mkoa wa Singida wakionesha kuwa wao ni sehemu ya mabadiliko kwani wanatoka kutafuta fursa kwa ustawi wa jamii yao.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.