Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI Mhe. Zainab Katimba (Mb) Amewasihi wananchi wa Manispaa ya Singida kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi anayetekeleza mradi wa TACTIC pamoja na kutunza miundombinu inayojengwa pale itakapokamilika ili iweze kuwa na tija iliyokusudiwa na kudumu kwa muda mrefu zaidi, akiziagiza Halmashauri zote zenye miradi ya TACTIC kusimamia vyema uendeshaji wa masoko na Vituo vya Mabasi ili kuzalisha mapato yaliyotarajiwa na Serikali kwa maendeleo ya maeneo yao.
Mhe.Katimba amesema kukamilika kwa utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) awamu ya pili Kwenye Manispaa ya Singida kutaleta mabadiliko chanya kwenye huduma, manunuzi na mazingira bora ya kufanyia biashara kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa Mkoa wa Singida.
Ameyasema leo Juni 2,2025 katika hafla ya utiaji saini Miradi ya Ujenzi wa Soko la Kimataifa la Vitunguu katika viwanja namba 835 na 836, Mtaa wa Misuna, lenye jumla ya mita za mraba 14,465. Jengo la ghorofa mbili, barabara za mzunguko zenye urefu wa mita 700 zitakazojengwa kwa kiwango cha lami,Ujenzi wa Barabara za Mjini Kati na Viwandani, zinazolenga kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na huduma na Ujenzi wa Mtaro wa Maji ya Mvua Mnang’una unaotarajiwa kuzuia mafuriko na kulinda mazingira ya mijini.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametumia jukwaa hilo kueleza dhamira ya Mkoa wa Singida kujiimarisha kiuchumi na kuchangia kwa kiasi kikubwa pato la taifa.
"Sisi ni majirani wa Makao Makuu ya nchi, Dodoma. Hivyo tumeamua kutumia nafasi yetu ya kijiografia kuwa mkoa wa mfano na kuwa jiji tarajiwa la kanda ya kati," amesema Mhe. Dendego.
Ameongeza kuwa, Mkoa wa Singida umeendelea kuwa mwenyeji mzuri wa wageni na wawekezaji, hasa baada ya kuwa mwenyeji wa Maadhimisho ya Kitaifa ya Mei Mosi, ambapo watu kutoka ndani na nje ya nchi walifika na kuvutiwa na fursa zilizopo akisema kuwa ushirikiano baina ya serikali, sekta binafsi na wananchi ndio nguzo ya mafanikio hayo.
"Sisi wana Singida tumeamua kupindua meza na kuwa mkoa bora Tanzania. Tuna kila sababu ya kufanikiwa; rasilimali tunazo, nia tunayo, na Mungu ametujalia ardhi nzuri, dhahabu, mazao ya chakula na biashara pamoja na mifugo," amesema Mhe.Dendego
Mhandisi Humphrey Kanyenye, Mratibu wa miradi ya Benki ya Dunia, TARURA amewataka Wakandarasi wazawa kujitokeza kwa wingi kuomba tenda mbalimbali za utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu ya Miji ya Tanzania (TACTIC) ili kuweza kunufaika na fursa hiyo kama sehemu ya kukuza uchumi wa Tanzania na kuimarisha mzunguko wa fedha nchini.
"Maeneo mengi tumepata wakandarasi wa Kichina lakini kwa Manispaa ya Singida tumepata bahati ya kupata mkandarasi mzawa na yeye pia amefanya kazi maeneo mengine na katika kulinganisha utendaji kazi wake kulinganisha na wakandarasi wa Kichina, Mkandarasi huyu yupo mbele kwa asilimia zaidi ya 20, “ amesema mhandisi Kanyenye.
Kulingana na mhandisi Kanyenye, kukamilika kwa mradi wa TACTIC kutaleta manufaa makubwa kwa Manispaa ya Singida ikiwemo kuongeza fursa za ajira, kuchochea ukuaji wa uchumi, na kuboresha hali ya biashara katika maeneo husika, hivyo kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya jamii na Taifa kwa ujumla.
Soko la Kimataifa la Vitunguu litajengwa mkoani Singida likitarajiwa kuwa na jengo la ghorofa mbili likiwa na eneo la kuchambua vitunguu, kukaushia vitunguu, maduka 10, Vyumba 4 vya huduma za kifedha, pamoja na maeneo mengineyo likitarajiwa kuongeza mapato ya Halmashauri kutoka Milioni 300 hadi Milioni 505 litakapokamilika.
Mradi huo unaotekelezwa na Mkandarasi mzawa M/s Sihotech Engeneering Company Limited kwa kushirikiana na kampuni ya AMJ Global Mult Contractors kwa gharama ya shilingi 24, 748,966,236.05 na unatarajiwa kukamilika mara baada ya kipindi cha miezi kumi na tano kitakachoanza Juni mwaka huu.
SINGIDA
Postal Address: P O BOX 5 SINGIDA
Telephone: 2502170, 2502089
Mobile: 2502170, 2502089
Email: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.