Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, akiambatana na Mwenyekiti wa CCM mkoq wa Singida sambamba na wajumbe wa kamati ya siasa Mkoa wameridhishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi ambapo wamekagua miradi mitatu ya kimkakati inayotekelezwa katika wilaya ya Iramba na Mkalama ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuimarisha huduma za kijamii na kuinua uchumi wa wananchi.
Mradi wa Skimu ya Umwagiliaji Msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama umeendelea kutekelezwa kwa kasi chini ya usimamizi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji. Mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni 34.1 unalenga kuwezesha umwagiliaji katika eneo la hekta 800 na kunufaisha zaidi ya wananchi 12,000 kutoka vijiji vinne vya Ishinsi, Ndurumo, Msingi na Kidi. Hadi sasa, utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 50 ambapo baadhi ya kazi muhimu zimeshakamilika, ikiwemo ujenzi wa ofisi ya meneja, barabara ya kuingia bwawani, na sehemu ya mfereji mkuu wa zege. Changamoto ya muundo wa tuta kutokana na hali ya udongo na maji mengi katika eneo hilo imeshughulikiwa kwa kushirikisha wataalamu wa miamba na usanifu wa mabwawa, na kazi zimeendelea kwa kasi.
Katika Wilaya ya Iramba, viongozi hao wamekagua mradi wa maji unaotumia bomba linalotoka Ziwa Victoria kupitia Nzega, Igunga hadi Shelui. Mradi huu ambao umeanza kutoa huduma tangu Agosti 2022 ukiwanufaisha wakazi 21,000 katika vijiji vya Shelui, Temu, Kizonzo na Gera, huku upanuzi unaoendelea kupitia RUWASA Mkoa ukiwa umeshakamilika kwa asilimia 96. Mabomba ya maji yenye urefu wa kilomita 16.14 yamesambazwa na vituo vitano vya kuchotea maji vimejengwa, ambapo wananchi wengine zaidi ya 7,900 wanatarajiwa kuunganishwa na huduma hiyo, hivyo kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama katika vijiji 70 na vitongoji 393 vya wilaya hiyo.
Aidha, viongozi hao wametembelea eneo la mradi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda hadi Tanzania (EACOP), ambapo shughuli za ujenzi katika maeneo ya Singida, hususan kijiji cha Ntondi kata ya Msisi, zimekamilika kwa asilimia 100.
Takribani kilomita 90 za bomba hilo zimepita mkoani Singida huku kipande kinachoanzia Tumuli (KP898) hadi Manyara (KP994) kikiwa na urefu wa kilomita 96.5. Ujenzi wa bomba hilo umekuwa chachu ya ajira kwa Watanzania, na vijana wengi wamenufaika kwa kupatiwa mafunzo maalum ya kitaalamu ili kushiriki kikamilifu katika fursa za kiuchumi zinazotokana na mradi huo wa kimkakati wa kikanda unaotarajiwa kukamilika robo ya tatu ya mwaka 2026.
Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mhe. Dendego amewapongeza wakandarasi kwa kazi kubwa waliyofanya licha ya changamoto mbalimbali, na amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha maeneo yote ya mradi yanakamilika kabla ya ujio wa Mwenge wa Uhuru. Aidha, amewataka viongozi wa vijiji na halmashauri kuanza kuwagawia wakulima maeneo yao na kuwapatia hati miliki ili kuondoa migogoro ya ardhi mara baada ya mradi kukamilika. Ameeleza kuwa ni muhimu kila mkulima ajulikane kwa eneo lake na apewe hati halali ili kuimarisha usalama wa miliki na matumizi ya ardhi kwa maendeleo endelevu.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Mhe. Martha Mlata, amepongeza kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo na kuwataka wananchi kuwa watulivu kuelekea Uchaguzi Mkuu, huku akisisitiza umuhimu wa kuchagua viongozi wenye uwezo wa kusimamia na kuendeleza miradi mikubwa ya maendeleo. Ameeleza kuwa ziara hiyo ni sehemu ya utaratibu wa chama kufuatilia utekelezaji wa Ilani na kuhakikisha kuwa Serikali inaendelea kutekeleza ahadi zake kwa wananchi.
Kwa ujumla, utekelezaji wa miradi ya kimkakati mkoani Singida umeendelea kuimarika na kuleta matumaini kwa wananchi, huku Serikali, chama na wadau mbalimbali wakishirikiana kuhakikisha kuwa miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kuanza kuleta matokeo chanya katika maisha ya wananchi na uchumi wa mkoa.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.