Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka madiwani pamoja na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida na Halmashauri ya Manispaa ya Singida kuhakikisha kuwa katika kila maamuzi wanayofanya wanajikita katika maslahi ya wananchi kwa kuwawakilisha kwa uaminifu na uadilifu mkubwa.
Ametoa rai hiyo wakati wa vikao maalum vya mabaraza ya madiwani kwa ajili ya kupokea taarifa za utekelezaji wa mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Amesema maamuzi yote yanapaswa kufanyika kwa kutanguliza dhamira njema kwa wananchi. “Katika siku zote unapofanya kazi, maamuzi utakayofanya, namna unavyofanya ile kazi, vaa kwenye viatu vyako, pima lile joto, ukiona kwamba linakubariki endelea kufanya, ukiona hata wewe unapata ukakasi, achana na mambo haya,” amesema RC Dendego.
Katika kikao cha Halmashauri ya Wilaya ya Singida, RC Dendego ameagiza watumishi wa halmashauri hiyo wanaodaiwa zaidi ya Shilingi milioni 6 walizokusanya kutoka vyanzo mbalimbali vya mapato lakini hawakuzifikisha benki, kuhakikisha wanazirejesha ndani ya siku saba. “Afisa Utumishi hao watumishi wanaodaiwa hizo fedha si wapo? Hatuna sababu ya kuendelea na hoja ya Shilingi milioni 6, ni kuichafua halmashauri, naagiza ndani ya siku saba watafute hizo fedha popote, ikigonga ile siku ya saba unakuja kunieleza kwa maandishi wameshalipa,” amesisitiza.
Kadhalika Amepongeza pia juhudi za madiwani katika kupigania maslahi ya wananchi na kuwataka waendelee na moyo huo huo kwa kuwa hoja zinazojadiliwa zinaathiri maisha ya kila siku ya mwananchi wa kawaida.
Katika Manispaa ya Singida, RC Dendego amesisitiza umuhimu wa ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 100 na kuonya kuwa wakuu wa idara ambao hawafanyi kazi kikamilifu watahamishiwa vijijini. “Kukaa mjini ni fursa, na kama hufanyi kazi tutakupeleka kijijini,” amesema. Pia ameagiza Katibu Tawala wa Mkoa kuitisha mkutano wa dharura na kamati ya mikopo ya wanawake, vijana na walemavu kwa ajili ya kubaini changamoto zilizopo na kuzitatua haraka. “Tusikae kiboss, tukae kama wahudumu,” ameongeza.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amepongeza juhudi za halmashauri hizo kwa namna wanavyoshughulikia hoja za CAG kwa weledi na bidii. Ameeleza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Singida imeonekana kuwa na idadi ndogo ya hoja ikilinganishwa na halmashauri nyingine mkoani humo, jambo linaloashiria ufanisi wa watendaji wake.
Katika Manispaa, Daktari Mganga amehamasisha matumizi ya fursa zilizopo kwa ajili ya kuongeza mapato na kupendekeza kuanzishwa kwa SPV (Special Purpose Vehicle) ya kusimamia miradi ya maendeleo ya kimkakati mjini Singida.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Mhe. Elia Digha, amesema kuwa tangu aingie madarakani hoja zilipungua kutoka 150 hadi 27, ambapo 19 zimefungwa na 8 ziko katika hatua ya mwisho. Amesema hoja za zamani zilikuwa 17 na hadi sasa 10 zimefungwa na 7 zimebaki.
Ameeleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya kazi ya pamoja ya viongozi na watendaji, na kuwataka waendelee kushirikiana hata katika kipindi cha uchaguzi mkuu kinachokuja, akisisitiza kuwa huduma kwa wananchi haina msimu.
Kwa upande wa Manispaa, Meya wa Singida, Mhe. Yagi Maulidi Kiaratu, amewataka madiwani kutafuta suluhisho la hoja zilizobaki kwa lengo la kuiwezesha halmashauri hiyo kuondokana na changamoto za ukaguzi na kuongeza uwajibikaji.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Bi. Joanfaith Kataraia, amesema kuwa Manispaa hiyo imepokea hati safi kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Amesema hoja 64 zilijadiliwa, 47 zikafungwa, 5 ni za kisera na 12 ziko kwenye hatua za utekelezaji. Halmashauri inaendelea na zoezi la kufunga hoja hizo kwa ukamilifu.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, amepongeza juhudi za halmashauri zote mbili na kuhimiza kuendelea kupunguza hoja kwa kufuata mapendekezo ya ukaguzi na kutumia vyema fedha za serikali. Amesisitiza kuwa fedha zisipotumika kwa mujibu wa sheria, hurudi Hazina Kuu, hivyo ni muhimu watendaji kufanya kazi kwa bidii ili fedha za maendeleo ziwafikie wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, amesema kuwa wamejipanga kufanikisha makusanyo ya mapato kwa asilimia 100 kama alivyoelekeza Mkuu wa Mkoa. Amepongeza pia wanasheria wa halmashauri kwa kazi nzuri ya kushughulikia kesi mbalimbali za halmashauri, akibainisha kuwa usimamizi wa fedha za umma ni jukumu la kila mmoja.
Kwa ujumla, mikutano hiyo ya mabaraza ya madiwani imeonesha dhamira ya dhati ya viongozi wa Mkoa wa Singida katika kuhakikisha uwajibikaji, usimamizi thabiti wa fedha za umma, na ufanisi wa utendaji kazi ndani ya halmashauri kwa lengo la kuwaletea maendeleo wananchi wa Singida.
SINGIDA
Anuani: P O BOX 5 SINGIDA
Simu: 2502170, 2502089
Simu: 2502170, 2502089
Barua Pepe: info@singida.go.tz ras@singida.go.tz
Copyright ©2023 Singida Regional Commisioner' Office . All rights reserved.